Wednesday, April 24, 2013

((((((I HURT MY MOM!!)))))) STORY FUPI ZENYE MAFUNZO MAISHANI

Mama yangu alikuwa na jicho moja, nilikuwa namchukia sana, kwa ufupi alikuwa kero sana kwangu. Mama alikuwa mpishi katika shule niliyokuwa nasoma, ilikuwa ni shule iliyojengwa maalumu kwa ajili ya watoto yatima. Pengine waweza kujiuliza kwa nini nilikuwa nasoma pale wakati nilikuwa na wazazi? Ukweli ni kwamba baba yangu alikuwa amefariki miaka mingi wakati mie bado mtoto mchanga. Mama aliomba kazi ya upishi katika shule ile ili apate pesa za kunitunzia mimi wakati huo maana baada ya kufariki baba ndugu walimpora mali zake zote na kumfukuza katika nyumba yake, hivyo ndiyo sababu iliyopelekea mama kuomba kazi ya upishi katika shule ile ili apate kujikimu kimaisha. Kama nilivyokwambia hapo awali kwamba kutokana na jinsi alivyokuwa mama nilikuwa simpendi kabisa. Mama yangu yeye alikuwa ananipenda sana na alijitahidi kunipenda sana lakini sikujali hayo, kwani alikuwa ananikera sana na ile hali ya kuwa na jicho moja.

Mama alikuwa ananitembelea kila mara wakati wa mapumziko alikuwa akijisikia raha sana kuniona mwanae nikiwa ana furaha wakati wote, lakini tofauti na hapo nilikuwa nakosa amani sana kila alipokuwa akitokea tu. Basi mama wakati mwingine ilimbidi asije kunisalimia maana alikuwa hapendi kuniudhi. Siku moja baada ya juma moja kupita mama alikuja kunitembelea na kutaka kunijulia hali, nilipomwaona tu nikakunja sura kuonyesha kukasirishwa na ule ujio wake. Nikawaza moyoni mwangu na kusema “Hivi huyu mwanamke kwa nini ananifanyia hivi?” ina maana yeye anajisikia raha kunikosesha amani. Mama aliponiona tu alitabasamu na kunifuata ….. mmoja kati ya wanafunzi wangu alicheka na kusema “ Eeeee muone mama yakooo ana jicho moja” Maneno yale yalizidi kuongeza kichwani mwangu nilitamani ardhi ipasuke niingie na inifunike. Na wakati mwingine nilitamani mama atoweke kabisa nisimuone maishani mwangu. Mama aliposogea karibu yangu nilimtwanga swali “Hivi wewe mwanamke unanipenda kweli?” mama yangu akajibu “Ndioo mwanangu nakupenda sana tena zaidi ya sana kwani wewe ni mtoto wangu pekee na sina mtoto mwingine zaidi yako, wewe ni lulu moyoni mwangu na dhahabu machoni pangu na wewe ndio furaha ya maisha yangu” kwa hasira huku nikifoka nikamwambia kama kweli unanipenda kwa nini usife ili mimi nikawa na raha hapa duniani?. Mama yangu hakujibu kitu kwa wakati ule….

Akaamua kuondoka machoni pangu kimya kimya! Mimi wala sikuona kama lile lilikuwa kosa na wala sikufikilia na wala sikupata walau hata nukta moja ya kutafakari nini ninachokifanya, sababu nilikuwa nina hasira sana. Ukweli nilikuwa sitambui mawazo yake mama na nilikuwa sijui nini mama anavyowaza juu yangu. Na kwa vile sikuwa na lakumfanya kwa wakati ule baada ya yeye kutoka mle ndani nami nikatoka nje huku nikiwa na mawazo sana. Nilikuwa nasoma kwa bidii sana, na baada ya mtihani wa mwisho nikapata bahati ya kuchaguliwa kuendelea na masomo ya juu jijini Dar es salaam. Hivyo kwa nguvu ya shule nilisafirishwa kutoka Mbeya mpaka dar, mama alinipatia pesa za matumizi pindi nitakapokuwa dar! Kwa jinsi alivyokuwa ananipenda alinipa mshahara wake wa miezi mitano, kumbe alikuwa ananitunzia hata kabla matokeo hayajatoka. Nilifurahi sana ingawa sikumshukuru lakini mama hilo hakujali alifurahi sana vile ambavyo nilipokea zile pesa kisha akanitakia safari njema. Nilipofika dar nikaendelea na masomo yangu kama kawaida. Kwa bahati pia nikafauru vizuri kisha nikaajiliwa Serikalini, Maisha yangu yalikuwa mazuri sana. Nilijenga nyumba nzuri ya kifahari nikanunua gari ya kutembelea ilikuwa gari aina ya Land cruzer mayai.

Sio siri maisha yangu yalikuwa mazuri sana. Baadaye nikaamua kuoa mke, tukazaa watoto watatu, familia yangu ilikuwa na furaha sana, sikuacha kuwasiliana na walimu wangu wa mbeya katika ile shule ya watoto yatima niliyokuwa nikisoma hapo awali, na kwa vile kwa wakati huo nilikuwa na pesa za kutosha nilikuwa natuma misaada katika shule ile. Ila mama sikuwahi kutuma hata shilingi kumi. Kwani nilikuwa natamani afe ili asiendelee kunitia aibu. Mama baada ya kupata habari kuwa mwanae maisha yangu yamekuwa mazuri na pia alisikia kuwa nimeoa na pia nimezaa watoto alifurahi sana na alitamani sana kuwaona wajukuu zake. Kwa wakati huu mama yangu alikuwa ameanza kuzeeka na aliamua kuacha kazi yake ya upishi katika ile shule. Pamoja na kuwa alikuwa ni wanamke aliweza kujijengea kakibanda ka kujisitiri na kwa vile alikuwa ameitumikia shule kwa muda mrefu hawakuacha kumtunza, pia waliendelea kumpa mshahara wake kama kawaida maisha yakawa yanasonga. Kwa upande wangu sikutaka hata kusikia habari zake. Siku moja mama akaamua kunifuata Dar, ili walau awaone wajukuu zake na hata mie mwanaye kwani alikuwa hajaniona zaidi ya miaka ishirini na mbili hivi, akapanda basi na kuja dar kwa bahati alipofika dar alimpata msamalia mmoja aliyeweza kumsitiri kama mjuavyo jiji la dar jinsi lilivyo na zamani ilikuwa kutoka mbeya hadi dar unatumia siku mbili na kwa vile alikuwa amefika usiku hakujua ni wapi aelekee.

Siku iliyofuata aliamua kunitafuta kwa kuulizia na kwa vile mimi nilishakuwa mtu maarufu sana hakupata shida kuipata nyumba yangu. Alipofika Getini alibisha hodi, na mlinzi baada ya kumhoji na kupata maelezo alimruhusu aingie, alipokuwa akikaribia mlango wangu, niliwasikia watoto wangu wakipiga kelele huku wakimcheka mama yangu na kusema “Heee! Cheki hicho kibibi kizee chongo kimekuja kwenye birthday party ya baba bila kualikwa” kusikia hivyo nkatoka nje na nikamuona mama akija wakati huu alionyesha wazi kuwa alikuwa mdhaifu! Ingawa hatukuonana kwa muda mrefu sana, sikuwa na hata chembe ya kumkumbuka. Nilifoka na kumwambia “ We kizee wewe unathubutuje kuja humu ndani na kuwashitua watoto wangu? Hauna hata haya tafadhari sana naomba uondoke haraka hapa.” Tokaaa!! Mama aliniangalia kwa huruma sana huku machozi yakimlengalenga katika macho yake, kisha akasema “Samahani kijana wangu nimekosea nyumba aliyenielekeza alinielekeza vibaya! Naomba unisamehe sana! Akageuka na kuanza kuondoka, haimaanishi kuwa hakunitambua alifanya vile ili kuuridhisha moyo wangu!.. hivyo akatoweka machoni pangu wala kuumia moyo kwa mama sikupata shida. Mama alikwenda moja kwa moja stendi ya mabasi kukata ticketi ya kurudi mbeya. Wakati ule ilikuwa manazi mmoja.

Akalala kwenye basi kesho yake akaanza safari ya kurudi Mbeya. Siku moja nilipokea barua kutoka katika ile shule niliyokuwa nikisoma ya watoto yatima, wakinihitaji niende huko kulikuwa na sherehe iliyoandaliwa ya kuwakutanisha wanafunzi wote waliosoma miaka ya nyuma ambao wamekuwa bega kwa bega katika kuisaidia shule ile. Kwa hiyo hata mie nilikuwa mmoja wao, na kwa vile nilijua kuwa nakwenda ni nyumbani sikutaka mke wangu amfahamu mama yangu na pia sikutaka mke wangu ajue kuwa nilisoma shule ya watoto yatima hivyo nikamuaga kuwa naenda Mbeya kikazi kwani siku zote mke wangu nilimwambia kuwa mie ni mzaliwa wa Dar na sina ndugu kabisa wazazi wangu wote wawili walifariki zamani sana. Siku iliyofuata nikaanza safari yangu kuelekea nyumbani kwetu mbeya, wakati huu nilikuwa nawaza jinsi ambavyo ningepokelewa kwa furaha pale shuleni lakini nilikuwa napata shida sana kwamba naenda kukutana na mama yangu ambaye alikuwa kero sana kwangu. Sikumpenda sana mama yangu hasa kwa lile tatizo lake la kuwa na jicho moja. Nilifika salama mbeya na kwa vile nilikuwa nimetumia usafiri wangu nilifika mapema kabisa, nikaenda katika moja ya nyumba za kulala wageni iliyokuwa bora sana nyumba yenyewe ilikuwa ikiitwa Mount Livingstone Hotel. Basi kama ilivyo ada nikaamka asubuhi na kujiandaa tayari kwenda kwenye sherehe.

Nilipofika kwenye sherehe kulikuwa na maclassmet kibao walikuwa wamefika pale na pia walikuwa na wake zao na hata wale waliokuwa ni madada zetu walikuwa wamekuja na waume zao, pamoja na hayo yote walikuwa wamekuja na wazazi wao karibu kila mmoja alikuwa na mzazi japo mmoja. Kwa upande wangu nilikuwa peke yangu, zaidi sana nilikuwa nimeambatana na dereva wangu tu. Lakini halikunipa shida hilo na nilikuwa nimeshukuru sana mama yangu kutokuwepo pale kwenye sherehe. Sio siri sherehe ilikuwa imefana sana na ilikuwa ni ya aina yake. Baada ya sherehe tukaendelea kusalimiana na wale wazee wa pale kijijini wote tukiwa na furaha sana. Baadaye akaja yule mama aliyekuwa rafiki yake na mama yangu akaniambia “pole sana mwanangu kwa msiba wa mama yako” Msiba wa mama? Nilimtwanga swali kuonekana kana kwamba nimeshituka, ingawa nilijua wazi yule mama alikuwa anajua tabia yangu na yale yote niliyokuwa nikimtendea mama yangu! Yule mama akasema “ndioo mama yako alikufa mwezi week mbili zilizopita ina maana hukupata taarifa? Nikamjibu sikupata taarifa. Basi tuakaendelea na mazungumzo mengine, ila kusema ukweli ile taarifa ilinifurahisha moyoni mwangu nikajua kuwa kero yangu sasa imekwisha. Hata hivyo mwisho wa mazungumzo yule rafiki wa mama yangu aliniita pembeni na kuniomba niambatane naye kwenda nyumbani kwake, nami bila hiyana nikakubali kwenda.

Tulipofika nyumbani kwake aliingia chumbani kwake na kutoka na barua akanipatia ile barua na kuniambia kuwa mama yangu alisema anipatie mimi….. Nilipokea ile barua kuanza kuisoma ilikuwa imeandikwa hivi:- Kwa Mwanangu Kipenzi, Nimekuwa nikikuwazia wewe wakati wote, sababu nakupenda sana, Naomba unisamehe sana kwa kuwatisha watoto wako siku ile niliyokuwa nimekuja kwako Dar, naomba nisamehe sana mwanangu, nisamehe sana. Nimepata furaha sana kusikia kuwa utakuja huku kwenye sherehe ya shule yenu, lakini najua kuwa sitakuwepo kwenye sherehe hiyo, kwani sipendi kukukwaza mwanangu. Ila mwanangu najua nimekukwaza kwa muda mrefu lakini haikuwa malengo yangu ilikuwa ni kwa sababu ya upendo niliokuwa nao kwako na vile nilivyopata tabu sana kukupata kwani wewe ndiwe mtoto wangu wa pekee. Sikia mwanangu…… nataka ufahamu haya… Wakati ukiwa angali bado mdogo ulipata ajali na kupoteza jicho lako moja na mimi kama mama yako sikupenda kukuona mwanangu ukikua huku ukiwa na jicho moja hivyo nikaamua kutoa jicho langu moja na kukuwekea wewe, ili ukue huku ukifurahia ulimwengu huu mpya ukitumia kiungo changu ambalo ndiyo jicho nililo kupatia. Nilikupenda sana mwanangu nab ado nakupenda sana! Ni mimi mama yako!! Mwisho!.. NB: Ni stori tu ila kuna watu wana tabia za kuwadharau wazazi hususani mama zao naomba kwa hali yoyote ile mpende mama yako, hakuna aliye kama mama hapa Duniani!!! Nampenda sana mama yangu

2 comments: